Unapoamua kupenda, vaa uvumilivu, ikibidi kubali kuwa bwege
Mada hii ina lengo la kukufanya uyaelewe mapenzi. Si kukimbilia kuacha pale kunapotokea tofauti za hapa na pale na mwenzi wako wa maisha. Uvumilivu unahitajika, amini kwamba utamu wote unaoyazunguka ‘malavidavi’ kuna ugumu mkubwa.
Ni sehemu ya tatu. Hapa tunazungumzia elimu zaidi inayoweza
kukukomboa wewe kwa kuheshimu hisia za mwenzako na wakati huohuo ukawa
unajali za kwako. Kwa pamoja ndipo utaweza kufanikiwa kuwa na moyo
tulivu katika nyakati zote.
Ukiheshimu hisia za mwenzi wako na ukawa unajali za kwako,
itakusaidia kukufanya uwe na tumaini chanya wakati wote. Wakati wa
matatizo, hasa kipindi ambacho hampo kwenye maelewano mazuri, utabaki na
imani kwamba yote yatakwisha.
Penda kuamini kuwa “hili nalo litapita” kwamba wakati ambao mwenzi
wako amenuna, hataki kuzungumza na wewe, unachopaswa kufanya ni
kuheshimu hisia zake na uamini kwamba mwisho atatulia na uhusiano wenu
utaendelea kwa maelewano makubwa.
Ukitaka kulazimisha awe mchangamfu kwako kipindi ambacho amenuna, ni
sawa na kukaribisha matatizo zaidi. Ni vema kuelewana, watu wengi
wanakosea katika uhusiano wao kwa sababu hawatumii busara ili kuwaelewa
wenzi wao pindi wanapoonesha hali tofauti.
Busara iendelee kuchukua nafasi. Maneno “hili nalo litapita” yawe
somo kwako. Kwamba leo umerudi nyumbani, umetaka chakula cha faragha,
mwenzako amekwambia hajisikii vizuri. Hutakiwi kupandisha mizuka na
kusababisha nyumbani pasilalike kwa siku hiyo.
Badala yake unapaswa kuvumilia. Jiulize mmefanya tendo mara ngapi
katika uhusiano wenu, iweje siku hiyo akwambie hajisikii? Ukilazimisha
ni sawa na kumfanyia mwenzako ubakaji. Si ajabu akiona unakuwa mkali,
akakubali kukupa kwa shingo upande lakini si kwa ridhaa yake.
Mapenzi ni matamu lakini siyo rahisi kwa maana nyakati nyingine
utalazimika kuvumilia mambo ambayo pengine yakakuumiza. Mpo wawili na
kujenga tafsiri ya mwili mmoja. Pengine hata makundi yenu ya damu ni
tofauti. Ilivyo maumbile yenu ni hasi na chanya ndiyo na damu zenu
zilivyo.
Tofauti hiyo mnaielewa na kuikubali, iweje siku ukirudi nyumbani
unamkuta amenuna na hataki kuzungumza na wewe ushindwe kuelewa? Hapo
ndipo uvumilivu wako unahitajika. Ni kipindi ambacho busara zako
zinapaswa kufanya kazi kwa asilimia 100. Usilazimishe afanye upendavyo
wakati mwili wake haupo tayari.
Unaingia faragha na mwenzi wako. Ameshindwa kukuridhisha kabisa. Ni
hekima zako kutambua kwamba siku hazilingani. Mbona siku nyingine
alikupa mambo mazuri mpaka ukasema ‘poo’? Tatizo ni nini? Pengine
nishati za mwili wake kwa siku hiyo hazipo sawasawa na hata yeye
mwenyewe hajui.
Ukimkejeli kuwa hajiwezi ni sawa na kumchinjia baharini. Siku
zinazokuja atashindwa kabisa. Si kwa sababu uwezo wake ni mdogo, la
hasha! Maneno yako ya kejeli na dharau ndivyo vitakavyoufanya moyo wake
usinyae na kukuogopa ndani kwa ndani. Fikra zake zitashambuliwa na
ugonjwa hatari.
Si ugonjwa unaosababishwa na kirusi, hapana. Ni gonjwa la maneno
litakaloshambulia ubongo wake. Kila mara kabla ya kuingia mchezo atakuwa
na maswali ya kujiuliza: “Sijui leo nitashindwa tena?” “Nikishindwa
itakuwaje?” “Atanitukana tena?” “Hivi mimi ni mgonjwa?”
Mwisho wa maswali hayo atahitimisha kauli kwa kusema: “Inawezekana mimi ni mgonjwa kweli ndiyo maana nashindwa kazi.”
No comments:
Post a Comment